MWANAFUNZI wa kidato cha nne Rebeka Maganga (17) anayesoma Shule ya Sekondari Old Shinyanga amedaiwa kufariki dunia kwa kujinyonga ndani ya chumba alichokuwa akilala nyumbani kwao alikokuwa akiishi na babu yake Mshala Peter (56).
Mwanafunzi huyo alijinyonga kwa kutumia mkanda wa sketi yake kisa kikidaiwa kukosekana shuleni wiki mbili bila taarifa nakutakiwa na walimu kwenda kumuita mzazi.
Kamanda wa jeshi la polisi mkoani Shinyanga Janeth Magomi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo juzi majira ya saa saba mchana katika eneo la kata ya Old Shinyanga ambapo mwanafunzi huyo alikuwa akiishi.
Kamanda Magomi amesema uchunguzi wa awali unaonesha kuwa marehemu alitumia mkanda wa sketi ya shule kujinyonga na kisa chake ni kukosekana shuleni kwa muda wa wiki mbili nakutakiwa na walimu akamuite mzazi.
“ Tunavyoona tukio la mwanafunzi kujinyonga limetokana nikuwa na msongo wa mawazo baada ya kurudishwa nyumbani na walimu kufuatia kutohudhuria masomo kwa muda wa wiki mbili bila taarifa”amesema Kamanda Magomi.
Kamanda Magomi amesema malezi ni jambo la msingi wanasikitika kuona mtoto huyo kulelewa na babu pekee huku wakishauri wazazi kutowatelekeza watoto hivyo aliwapongeza walimu kuwa na ushirikiano na mlezi huyo.
Mwenyekiti wa kitongoji cha Senyenge Kijiji cha Old Shinyanga Benjamin Andrew amesema walipokea taarifa za tukio hilo majira ya saa sita mchana na kufika eneo la tukio ambapo walimkuta mwanafunzi huyo ananing’inia amefariki.
Andrew amesema mwanafunzi huyo alikosekana shuleni kwa muda wa wiki mbili na walimu walimtaka arudi nyumbani akamuite mzazi ambapo alikuwa akiishi na babu yake .

0 Comments