Shinyanga
JESHI la polisi Mkoani Shinyanga limewashikilia watu 63 wakiwa na vielelezo mbalimbali ikiwemo kielelezo cha mafuta ya dizeli lita 295 na pikipiki 14.
Kamanda wa jeshi la Polisi Mkoa hapa Janeth Magomi amewaeleza waandishi wa habari leo kuwa katika oparesheni mbalimbali zilizofanyika kwa kuanzia mwezi April mwaka huu ilikuwa na lengo la kubaini na kuzuia uhalifu.
Kamanda Magomi amesema msako mkali ulifanyika na wameweza kuwashikilia watuhumiwa 63 wakiwa na makosa mbalimbali ambapo vielelezo walivyokamatwa mojawapo ni lita 295 za mafuta ya dizeli na pikipiki 14.
Kamanda Magomi amesema vitu vingine walivyo kamata ni noti bandia zenye thamani ya shilingi 81,000,simu za mkononi 98 na betri za simu 86.
Kamanda amesema wamefanikiwa kukamata pia vipande 21 vya chuma ,Redio nane,viti vya plasitiki sita,mifuko 13 ya mawe yadhaniwayo kuwa na madini, Spika tano,mashine ya kuoka mikate moja na mbuzi saba .
Wakati huo huo Kamanda amesema miongoni mwa watu 63 waliokamatwa wapo waliokuwa wanajihusisha na madawa ya kulevya ambapo walikamata Mirungi kilogramu 103,bangi kilogramu 1,100.
“Yapo mafanikio ya kesi saba zilizokuwa zimepelekwa mahakamani ambapo kesi tano za wizi washtakiwa saba wamehukumiwa kifungo cha kwenda jela miezi sita na wengine miaka minne na kesi moja kutishia kuua kwa maneno na kesi moja shambulio la kudhuru mwili na kuhalibu mali”amesema Kamanda Magomi.
Kamanda Magomi amesema tayari wamefanya mikutano 182 ya uelimishaji katika maeneo tofauti tofauti ikiwemo shuleni na vjiwe vya waendesha bodaboda ili jamii ielewe umuhimu wa kushirikiana na jeshi la polisi kutoa taarifa na ulinzi na usalama.

0 Comments