Na Kareny Masasy,
Shinyanga
MAMLAKA
ya maji safi na usafi wa mazingira Shinyanga (Shuwasa) imekuja na
mpango wa kutumia mita za malipo ya kabla(Prepaid meters) hatua
inayolenga kuondoa changamoto ya ulipaji wa bili hasa kwenye vituo vya
umma vya kuchotea maji ili kuongeza uwajibikaji kwa watumiaji.
Akizungumza
katika mkutano wa wadau wa maji safi wa kupitia rasmu ya mkataba
wa huduma kwa mteja ,Mkurugenzi wa Shuwasa Mhandisi Yusuph Katopola
amesema kufunga mita za maji za malipo ya kabla kwenye maghati
itawawezesha kuondoa usumbufu .
Katopola
amesema kuwa katika awamu ya kwanza zoezi hilo litaanza mwezi Aprili
kutekelezwa kwenye maeneo yenye changamoto kubwa ya ulipaji wa bili,
hususan kwa wateja wanaoshindwa kulipa kwa wakati au wanaolimbikiza
madeni ambao wanahudumiwa na Mamlaka hiyo.
“Tunajenga
magati ya maji ili kusaidia Jamii ya eneo hilo maana unapotekeleza
mradi ukishakamilika halafu wananchi wakakosa huduma mpaka wasubiri
kuunganishiwa inakuwa vigumu na ndiyo maana tunaweka maghati kusaidia
Jamii”amesema Katopola Mhandisi Katopola
Mhandisi
Katopola amesema mkataba wa zamani umeisha muda wake, na mamlaka hiyo
iko katika hatua za mwisho za kukamilisha rasimu ya mkataba mpya
utakaodumu kwa miaka mitatu kuanzia 2026 hadi 2029 baada ya kupitishwa
na Ewura.
Wadau wa sekta
ya maji akiwemo Anascholastika Ndagiwe wamepongeza Shuwasa kwa ubunifu
huo, wakieleza kuwa ni suluhisho la kudumu litakalosaidia kuboresha
huduma ya maji na kuongeza nidhamu ya matumizi kwa wananchi.
Mkuu
wa Wilaya ya Shinyanga Julius Mtatiro ametoa wito kwa Mamlaka ya
Majisafi na Usafi wa Mazingira Shinyanga kuzingatia kikamilifu mkataba
wa huduma kwa mteja pamoja na miongozo ya kisheria ili kuboresha utoaji
wa huduma .
Amesisitiza
suala la kufanya kazi kwa weledi na kutoa huduma bora kwa wananchi wa
Manispaa ya Shinyanga, huku akitaka kero zinazowakabili watumiaji wa
maji kutatuliwa kwa haraka na kwa ufanisi.



0 Comments