SERIKALI IMEPIGA MARUFUKU TAASISI NA WATU BINAFSI KUTOA MIKOPO UMIZA

Na Kareny Masasy,
Shinyanga

 SERIKALI  imepiga marufuku taasisi na watu binafsi wanaotoa mikopo kisha kuwafilisi mali za wakopaji bila kufuata taratibu za kisheri huku ikionya kuwa yeyote atakayebainika kufanya vitendo hivyo atakamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Julius Mtatiro alitoa kauli hiyo katika kikao kazi cha kujadili masuala ya mikopo kwa baadhi ya taasisi za fedha ambazo zimekuwa zikiwanyanyasa wananchi kwa kuweka masharti kandamizi kinyume cha sheria huku wakopaji wakilalamika kwa mikopo umiza.

Mtatiro amesema  ofisi yake haitasita kuchukua hatua kali dhidi ya taasisi au mtu binafsi anayetoa mikopo yenye riba kubwa isiyo halali huku akipiga marufuku vitendo vya kufilisi mali za wananchi kiholela mitaani.

“Katika Wilaya hii ya Shinyanga siwezi kuruhusu wananchi kunyanyaswa ni marufuku kwenda kufilisi mali za wakopaji wanapochelewa kulipa kuna taratibu za kisheria zinazopaswa kufuatwa  ikiwa ni pamoja na kufungua kesi mahakamani ili haki itendeke,” amesema Mtatiro

Baadhi ya wadau waliohudhuria kikao hicho  akiwemo  John shija alieleza  mikopo ya kausha damu imekuwa chanzo cha hofu kwa wananchi na migogoro katika familia huku wakopeshaji wakichukua  mali bila kujali madhara kwa wahusika.

Pia Shija amesema wanaponyang'anywa mali na kuwaacha watoto wakiteseka hali inayoongeza ugumu wa maisha kwa wahanga wa mikopo hiyo.

Mwenyekiti wa Mtaa wa Miti mirefu Nssoro Warioba amesema  hatua ya serikali kuingilia kati italeta unafuu kwa wananchi akibainisha kuwa tatizo hilo limekuwa likikua kwa kasi na kuhitaji udhibiti wa haraka.

Mwanasheria wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga Rose Matunda amesema  baadhi ya wakopeshaji wanafanya biashara hiyo bila vibali halali wakikiuka sheria na kutoa mikopo yenye riba zisizo na viwango vinavyoeleweka.

Matunda amesema  mikataba ya mikopo inapaswa kuwa wazi, yenye lugha rahisi inayomwezesha mkopaji na mdhamini kuelewa masharti yake, lakini hali hiyo haizingatiwi na baadhi ya wakopeshaji jambo linalotumika kuwanyanyasa wananchi.

Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga Peresi Kamugisha amesema upo umuhimu wa ufuatiliaji na usimamizi madhubuti wa sekta ya mikopo ili kulinda haki za wananchi na kuzuia vitendo vya unyonyaji vinavyoathiri ustawi wa jamii.


 

Post a Comment

0 Comments